Katuni.
Yanga iliyokuwa ugenini kwenye Uwanja wa Amahoro jijini Kigali,
Rwanda, iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji APR FC katika
mechi ya kwanza ya Raundi ya Kwanza ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika.
Azam FC walichomoza na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Bidvest
Wits mjini Johannesbrug, Afrika Kusini katika mechi yao ya kwanza ya
Raundi ya Kwanza ya Kombe la Shirikisho.
Wawakilishi pekee wa Zanzibar waliosalia kwenye michuano ya Afrika
mwaka huu, JKU FC wakitandikwa magoli 4-0 dhidi ya SC Villa ya Ligi Kuu
ya Uganda na kufifisha ndoto zao za kutinga Raundi ya Pili ya michuano
ya Kombe la Shirikisho.
Timu hizo zitarudiana Tanzania mwishoni mwa wiki hii, Yanga
wakiwakaribisha APR kwenye Uwanja wa Taifa, wakati Azam FC watakuwa
katika maskani yao yaliyopo Chamazi, huku JKU wakishuka kwenye Uwanja wa
Amaan visiwani Zanzibar.
Tukiwa wadau namna moja wa michezo nchini, Nipashe tunawapongeza
Azam FC na Yanga kwa kupambana na kupata ushindi ugenini licha ya
kucheza dhidi ya timu zenye uzoefu mkubwa wa mashindano ya kimataifa.
Mara nyingi viwanja vya ugenini vimekuwa vikionekana changamoto
kubwa kwa mafanikio ya timu za Tanzania ambazo zimekuwa zikitolewa hatua
za awali katika michuano ya kimataifa. Pengine msimu huu ni mzuri kwa
Wanalambalamba na Wanajangwani.
Rekodi ya juu kwa timu za Tanzania katika mashindano ya Afrika
ilikuwa 2003 Simba ilipotinga hatua na makundi na hatua kama hiyo
kufikiwa na Yanga mwaka 1998. Simba pia iliingia hatua ya fainali ya
Kombe la Shirikisho mwaka 1993.
Ushindi wa Azam na Yanga katika mechi za juzi umeonyesha njia ya
mafanikio kwa klabu za soka za Tanzania kimataifa, Lakini unahitaji
kulindwa nyumbani mwishoni mwa wiki.
Tunaamini ushindi huo wa ugenini si sababu kuntu kwa timu hizo
kubweteka na kuona tayari zimeshafuzu kutinga Raundi ya Pili kutokana na
ukweli kwamba wapinzani wao wanao uwezo wa kushinda ugenini.
Kutokana na ukweli huo, tunatoa rai kwa klabu za Azam na Yanga na
hata JKU kujipanga zaidi kwa mechi za marudiano kuhakikisha wanashinda
mechi za mwishoni mwa wiki dhidi ya wapinzani wao.
Tunafahamu kila timu imejiandaa, lakini siku zote tunaamini kuwa,
timu inayojiandaa kushinda nyumbani na ugenini ndiyo inayokuwa jirani na
mafanikio katika mashindano ya mtindo wa mtoano kuliko ile isiyofanya
hivyo.
Ndiyo maana tunasema Azam na Yanga bado hawajamaliza kazi Afrika
licha ya kupata ushindi katika mechi zao za ugenini Rwanda na Afrika
Kusini.
Tunaamini mipango mizuri ya mechi zao za marudiano, itakuwa sehemu
ya maandalizi yao ya mechi za hatua inayofuata ya Raundi ya Pili ya
Klabu Bingwa na Kombe la Shirikisho, ikizingatiwa kuwa watakutana na
timu kubwa. Yanga, kwa mfano, wakiing'oa APR, watacheza dhidi ya Al Ahly
ambayo iliwang'oa mwaka juzi.