Katuni.
Uchaguzi huo ulifanyika kutokana na matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa
Oktoba 25, mwaka jana kufutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar
(Zec), Jecha Salim Jecha, kwa madai kuwa ulijaa kasoro kadhaa.
Hata hivyo, uamuzi wa Jecha ulikosolewa na makundi kadhaa wakiwamo
waangalizi wa kimataifa wakisema katika ripoti yao ya awali kuwa ulikuwa
mzuri kuliko hata wa mwaka 2010.
Chama cha wananchi (CUF) ambacho ni chama kikuu cha upinzani
Zanzibar kilipinga maamuzi ya Jecha na kutangaza kutoshiriki katika
uchaguzi wa marudio kwa kuwa kinatambua uchaguzi halali ni uliofanyika
Oktoba 25, mwaka jana.
Kimsingi, kumekuwapo na mgawanyiko miongoni mwa Wazanzibari baada
ya tangazo la Jecha la kufuta matokeo hayo na kutangaza uchaguzi wa
marudio. Mgawanyiko huo umejikita zaidi katika itikadi za vyama vya CCM
na CUF.
Tunachukua fursa hii kumpongeza Dk. Shein kwa ushindi alioupata na
ni matumaini yetu kwamba atahakikisha kwamba anafanya kila liwezekanalo
kuinua uchumi wa Zanzibar sambamba na kuwapatia Wazanzibari wote
maendeleo.
Tunaamini kwamba hilo atalitekeleza kwa kuwa jana wakati akitoa
shukrani baada ya kutangazwa mshindi na kukabidhiwa cheti cha ushindi na
Jecha, alisema Zanzibar itatumia kila rasilimali iliyopo kuhakikisha
inajitegemea.
Hata hivyo, ni jambo lililo wazi kwamba Wazanzibari wamegawanyika
tena kutokana na kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi wa mwaka jana na ndiyo
maana CUF yenye wafuasi wengi hususani Pemba haikushiriki katika
uchaguzi wa juzi.
Kutoshiriki kwa CUF ni dhahiri kuwa Wanzanzibari wanaokiunga mkono
chama hicho watakosa uwakilishi katika vyombo muhimu vya maamuzi kwa
maana ya Baraza la Uwakilishi na mabaraza ya madiwani.
Baada ya kupatikana maridhiano mwaka 2010 na kuundwa kwa Serikali
ya Umoja wa Kitaifa (SUK) iliyovishirikisha CCM na CUF, Zanzibar ilipata
ululivu wa kisiasa na kumaliza uhasama uliokuwapo tangu kabla ya
Mapinduzi ya Zanzibar na ulioendelea baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa
vyama vingi vya siasa mwaka 1992.
Ushindi alioupata Dk. Shein na wagombea wa uwakilishi wa CCM
umeifuta SUK na hata kama itaundwa, haitakuwa na maana yoyote kwa kuwa
ukweli uko dhahiri kwamba serikali hiyo inaundwa kutokana na kuwapo na
CUF na siyo vyama vingine ambavyo havina wafuasi visiwani humo na ndiyo
maana hauina kilichopata asilimia 10.
Itakumbukwa kuwa kila uchaguzi tangu mwaka 1992 hadi 2010 CCM na
CUF vimekuwa vinatofautiana kwa idadi ndogo ya kura, hali iliyokuwa
inaonyesha kwamba hakuna chama cha kuunda serikali peke yake.
Kwa kuwa uchaguzi umefanyika kwa kufuata Katiba ya Zanzibar, hakuna
sababu ya kupinga matokeo yake, lakini ni lazima jitihada zikafanyika
ili kumaliza mgawanyiko uliopo kwani uchaguzi huo sio mwarobaini wa
mpasuko wa kisiasa unaoikabili Zanzibar.
Njia pekee ni meza ya mazungumzo ambayo itavishirikisha CCM na CUF
ambavyo vina wafuasi. Tunawaomba wale wote wanaojali maslahi ya Zanzibar
na Tanzania kwa ujumla. Bila Zanzibar yenye umoja, itakuwa vigumu
kuwapo maendeleo.
SOURCE:
NIPASHE