Katuni.
Wanajangwani walishinda 2-1 ugenini jijini Kigali wiki mbili zilizopita kabla ya juzi kulazimishwa sare ya 1-1 nyumbani dhidi ya timu hiyo ya Jeshi la Rwanda.
Kabla ya kuivaa APR, Yanga iliikabili Cercle de Joachim ya
Mauritius na kuitua nje ya michuano hiyo mikubwa zaidi kwa ngazi ya
klabu barani kwa jumla ya mabao 3-0.
Kwa kutinga raundi ya pili, Yanga sasa itakuwa na kazi ngumu
itakapochuana na Al Ahly ya Misri kwa mara nyingine baada ya msimu
mmoja.
Timu hiyo ya Ligi Kuu ya Misri iliing'oa Yanga katika michuano ya
Afrika mwaka juzi katika hatua ya matuta baada ya kutoka sare ya 1-1
katika muda wa kawaida, kila timu ikishinda nyumbani.
Takwimu za soka zinaonyesha timu za Tanzania zimekuwa zikitolewa
mara nyingi kwenye michuano ya Afrika na timu za kaskazini mwa Afrika
(za Kiarabu). Kutokana na ukweli huo, Nipashe tunaona kuna haja Yanga
kufanya maandalizi ya kina kabla ya kuwavaa Al Ahly.
Timu za Kiarabu zinasifika kwa kuwa na mipango mizuri ya nje na
ndani ya uwanja katika kusaka matokeo. Yanga wanapaswa kujipanga
kikamilifu kuhakikisha wanadhibiti mianya ya fitna za Al Ahly.
Na kama kweli wamedhamiria kulipa kisasi cha matokeo mabaya ya
mwaka juzi, tunafikikri Yanga wanapaswa kuanza maandalizi mapema kabla
ya kukutana nao.
Licha ya kufanya vizuri katika raundi mbili zilizopita, tunaamini
kikosi cha Yanga kinakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zisizofanyiwa
kazi mapema, zitakuwa na athari kubwa mbele ya nyota wa Al Ahly
wasiofanya makosa mengi wanapokuwa na nafasi ya kuifunga timu pinzani.
Katika mechi mbili zilizopita dhidi ya APR, kwa mfano, Yanga
imeruhusu mabao mawili na safu zake zote kuanzia ulinzi hadi
ushambuliaji zilionekana kuyumba.
Tunafahamu kuna changamoto ya kuwa na majeruhi kadhaa kikosini,
lakini Yanga ilisajili nyota 24 kwa ajili ya msimu huu ambao tunaamini
wakielezwa mbinu chafu na fitna za timu za Kiarabu, wanaweza kutinga
robo-fainali kwa kuing'oa Al Ahly na kuiwakilisha vyema Tanzania msimu
huu.
Al Ahly iliyoanzishwa Aprili 24, 1907 (miaka 28 kabla ya Yanga
kuanzishwa), ina rekodi nzuri katika mashindano ya Afrika, Timu hiyo
imeshinda mataji nane ya Ligi ya Mabingwa na moja la michuano ya Kombe
la Shirikisho.
Tunafahamu pia kuwa Al-Ahly ndiyo timu namba moja duniani kwa
kushinda mataji mengi ya kimataifa (Klabu Bingwa duniani) wakifanya
hivyo mara 20 na kuzipiku AC Milan, Real Madrid na Boca Juniors.
Lakini mpira unadunda, Yanga walikaribia kuing'oa mwaka juzi, tunaamini wanaweza kupata mafanikio hayo mwaka huu.
Ndiyo maana tunatoa rai kwa uongozi wa Yanga na benchi lao la
ufundi kujipanga vyema ili kupata matokeo mazuri nje-ndani dhidi ya timu
hiyo
SOURCE:
NIPASHE